27 September 2005

Upendo ni kila kila kitu.

Upendo ni kupenda. Unapopenda kitu hutaki kitu kile kipate madhara ya aina yoyote yale, na pale inapotokea kitu hicho kukumbwa na tatizo basi utafanya juu chini kuhakikisha unatatua tatizo hilo. Mwanao akiumwa utafanya juu chini kuhakikisha anarudia afya yake ya kawaida, unapogombana na Joe Tungaraza wako (mwandani) basi utahakikisha mambo mnayaweka sawa muda si mrefu hii yote ni katika kutaka kuishi kwa raha. Waswahili husema "penye upendo hapaharibiki neno".

Siku zote nimekuwa nikijiuliza ni kwa nini kuna vita, kwa nini kuna matabaka katika jamii zetu, kwa nini kuna rushwa, kwa nini kuna wivu usiokuwa wa maendeleo katika jamii zetu , kwa nini kuna migogoro isiyoisha.. Nimekaa nimefikiria sana na sasa nimepata jibu moja kwamba ni sababu ya ukosefu wa upendo.

Sisemi kwamba kwenye upendo migogoro haitokei hasilani..hapana migogoro hutokea lakini haidumu kwa muda mrefu na kuwa tatizo sugu. Sehemu yoyote yenye upendo watu hujaliana na kuthaminiana, humpenda mwenzie kama anavyojipenda yeye katu hatataka jirani yake apatwe na baya lolote na kama ikatokea mmoja akakumbwa na tatizo basi husaidiana kulitatua. Na huu ndio upendo wa kweli.

Sasa hivi tulio wengi hatuna upendo kabisaaa, si viongozi wa nchi, si raia si yeyote yule. Watu tumegeuka wabinafsi tunajipenda wenyewe tu, kama mtu mambo yako yakiwa swafi basi uhangaiki na mwingine kujua siku imemuendeaje, labda hakula au anauguliwa wewe hujui maadamu siku yako imepita vizuri yeye atajaza mwenyewe. Tukija kwa viongozi wetu....ma-ma-ma-maaa yaani hao ndio usiseme kabisa, kwa jinsi ninavyojua viongozi ndio kama wazazi wetu, husimama badala yetu sisi kama watoto wao na kuhakikisha hatupati matatizo yoyote kuanzia chakula, mavazi, malazi na mienendo ya tabia zetu. Lakini cha ajabu wazazi wetu hawa wamekosa upendo kabisa kwetu sisi watoto wao, wanakula wenyewe kwanza halafu ndio watoto, watoto wasiposhiba wenyewe hawajali, hawajui watoto wamelalaje au wameamkaje, wameenda shule au hawakwenda au wameacha kabisa hiyo wenyewe hawajui wanachojua ni kujishindilia wenyewe basi. Na mimi hili halinishtui kuona kwa nini watoto nao wanaamua kujiingiza katika makundi ya ujambazi na unyakuaji au tabia zozote potofu yote hii ni katika kujaribu kujisaidia maana wazazi wao hawajali. Ndio ni kweli watoto hujifunza kutoka kwa wazazi wao na kama mzazi haonyeshi upendo kwa wanae, watoto watajifunzaje upendo wa kumjali jirani yake?

Tanzania tuna watoto wengi wenye vipaji vya hali ya juu sana, lakini tunashindwa kuwaendeleza watoto wetu kwa vile vipato vyetu viko chini, na hatuwezi kumudu gharama za kuwalipia masomo. Sawa ni kweli lakini bado najiuliza hawa viongozi wetu wenye akaunti zao nchi za ulaya wanashindwa nini kujitolea angalau kila mmoja achukue watoto wawili tu na kuwasomesha? nina hakika hawatapungukiwa na kitu na huo ndio upendo ninaouongelea, hebu fikiria hawa matajiri wote wa Tanzania unaowafahamu wajitolee kusomesha watoto wasio na uwezo wa kifedha katika mashule yao ya akademiki ingekuwaje, nina hakika hawa watoto wasingechezea bahati wangeitwa John visomo. Na ni katika watoto hawa ndio tungepata vijana madhubuti wa taifa la kesho, tofauti na wengi wa watoto wa matajiri waliokulia katika fedha hawana shida ya kujishughulisha sana na masomo kwani fedha ipo na wanafikiri itakuwepo milele.

Haya, mimi sina mengi ya kusema lakini akili yangu inanituma kusema kwamba kama watanzania tutarudisha upendo kati yetu basi mabalaa yooote yanayotufuata fuata yatatafuta njia ya kutokea.

2 Comments:

At Thursday 29 September 2005 at 15:11:00 BST, Blogger mwandani said...

Upendo umo katika asili ya binaadamu. Chuki si asili bali msingi m-bovu. Ndio maana watu wote wanatahayari ukiwakamata wanafanya matendo ya kidhalimu. Ingawa chuki inaonekana kushamiri siku zote upendo unatumulika na tunatahayari. Endelea kupenda mwanao arithi hulka za upendo. Wema hauozi.

 
At Sunday 2 October 2005 at 15:20:00 BST, Anonymous Anonymous said...

Umetupa mpasho wa nguvu hapo. Hiyo ni falsafa.

 

Post a Comment

<< Home