15 September 2005

Hawatakaa wasahau.......

Ni mchana tulivu kabisa shuleni Nganza sekondari, wakati huo nikiwa kidato cha nne na mdogo wangu Mama Oprah kidato cha tatu. Tumekaa darasani tukijisomea huku tukisubiri kengele ya chakula igongwe wasichana tukapate ugali maharage, mara badala yake tunaona darasa zima la kina Mama Oprah linatolewa nje na kupigishwa magoti uwanjani, punde si punde ofisi nzima ya waalimu inatoka kila mwalimu akiwa na fimbo kadhaa mkononi...... heee! kulikoni tena mbona form three wamefanya nini?

Kisa chenyewe ndio hiki..., Mwalimu ???(wa kiume) alikuwa darasani akifundisha kama kawaida, Mwalimu huyu ukimwangalia tu utasema sijui aliumwa nini alipokuwa mtoto, uso wake una vijishimo vidogo na vikumbwa, ugonjwa huu uliompata utotoni ulimuathiri hadi ulimi wake ukawa mzito kuongea inabidi umzoee ili umwelewe kwa wepesi.

Sasa wanafunzi darasani, njaa imeshawakamata masikini ya Mungu, hawamsikilizi tena mwalimu bali wameanza kumkagua juu hadi chini. Mmoja akakata kikaratasi akaandika kitu fulani, akampasia mwenzie chini ya deski, akasoma akacheka kwa chini chini, akampasia na mwingine naye hivyo hivyo baada ya kusoma akacheka na kumpasia mwenzie, kazoezi haka kaliendelea bila mwalimu kujua kitu chochote, wanafunzi sasa karibu wote wanacheka chini chini, mwalimu akastukia kitu lakini akauchuna na kuanza kuwategea ili kujua ni nini kinachoendelea... watoto nao bila kujua wanaendelea kupasiana kikaratasi....mara ghafla mwalimu akamnyaka mmoja akimpa mwenzie....hapo hapo mwalimu akakiomba kikaratasi... akapewa yaani hapo darasa zima ni kama limemwagiwa maji... mwalimu akasoma kikaratasi looooh!! kinasema "uso wa mwalimu??? kama nyama ya ini". Jazba iliyompanda pale sipati kusema alitoka nje moja kwa moja ofisini akawakabidhi waalimu wenzie wasome....kilichoendelea hapo Bugando hospitali ndo inajua...... zilipita fimbo balaa ......lilikuwa ni fundisho.

1 Comments:

At Sunday 2 October 2005 at 15:23:00 BST, Anonymous Anonymous said...

Visa vya namna hii vinakumbusha mbali sana...

 

Post a Comment

<< Home