12 September 2005

Hatukujitokeza.

Bado tunasua-sua kina mama katika kutaka kushika usukani wa kuiongoza nchi yetu. Kama inavyojulikana kwamba mwezi ujao ndio uchaguzi mkuu wa kumchagua dereva wa nne wa kuikamata nchi yetu, ni mwanamke mmoja tu aliyejitokeza kugombea nafasi hiyo, tena si kwa kupenda mwenyewe bali ni kwa vile hakuna mwanamke aliyejitokeza. Yeye mwenyewe anakiri kwamba kama wanawake wakongwe kwa siasa wangegombea basi yeye katu, asingedhubutu kugombea,lakini kwasababu wamegwaya basi hakuwa na jinsi. Huyu si mwingine bali ni bibi Anna Claudia Senkoro. Lakini pamoja na hayo tunampongeza kwa uthubutu wake, amefungua njia.

Nilikuwa naongea na mshikaji wangu mmoja,juu ya suala hili la uongozi wa nchi kwa wanawake, akasema ingependeza sana na kungetokea mabadiliko makubwa kama Tanzania ingeongozwa na upande wa pili wa shilingi, akasema ukitaka kujua mwanamke hateteleki katika masuala ya uongozi basi mwangalie jinsi anavyoiongoza nyumba yake, tena tafuta yule mwanamke ambaye ana mume jina, ambaye akitoka leo uhesabu siku tatu ndo utamuona. Mwanamke huyu kwa vile ameshajua hana msaada wowote, basi atafanya kila aliwezalo kuhakikisha mambo hayaharibiki wa kuadhirika, mtakula, mtavaa na mtasoma. Akasema kwa ufupi mwanamke si mbinafsi, hufikiria kwanza watu wake halafu ndio yeye. Kwa hiyo kama mwanamke huyu akikamata madaraka ya kuiongoza nchi hatashindwa kwa vile ameumbwa na utu na uwezo wa kuongoza.

Nikamuuliza mbona kuna wanawake wengi ambao wanaongoza hadi sasa lakini hatuoni badiliko lolote ?...akasema hao wako chini ya vivuli juu yao kuna wanaorekebisha mambo, lakini kama kweli mwanamke mwenyewe ndio akawa Top macho yote yanamwangalia yeye basi ndo utamjua.

Nikamuuliza tena kwamba pamoja na sifa zote hizo za uwezo wa kuongoza kwa mwanamke, lakini bado kuna huu udhaifu wa kuona huruma na woga wa kuyakabili matokeo ya siasa kama kwenda jela na vitu kama hivyo... akasema hilonalo ni tatizo kubwa maana siasa ni kujitoa muhanga hasa, ni lazima uwe na roho kama ya malkia Sheeba au malkia Nzinga.

Baada ya maongezi hayo, binafsi nikaanza kupata picha, ya kwa nini tunasita sita katika kukamata madaraka ya juu, kwamba tunasumbuliwa na uzuri, hatutaki kuaibika, kuzomewa wala kukataliwa...aibu hiyo itupitie mbali kabisaaa, pili hatutaki kuteseka kama kwenda jela pale utakaposema ukweli.

Kina mama hebu tukae na tujiulize tena na tena,hadi lini tutakuwa tukisumbuliwa na tatizo hili la woga na kujipenda mno? Ninaamini nguvu ya uongozi tunayo sema hiyo minyororo ya utumwa tuliyojifunga wenyewe ndo inatumaliza.

Jamani tusaidianeni kuifungua tuwe huru.

0 Comments:

Post a Comment

<< Home